Skip to main content

KISWAHILI FORM 1: FASIHI KWA UJUMLA

KISWAHILI Form 1 Topic 3

FASIHI KWA UJUMLA
Mada hii ni utangulizi tu juu ya fasihi. Katika utangulizi huu utaelewa dhana ya fasihi, utajifunza juu ya kazi za fasihi katika maisha ya mwanadamu. Utajifunza juu ya tanzu (aina) za fasihi kwa ujumla wake. Kisha utajifunza sifa na dhima za kila tanzu ya fasihi kwa umahususi wake na mwisho utaweza kujifunza juu ya tofauti na uhusiano wa tanzu hizo za fasihi.
Dhana ya Fasihi
Elezea dhana ya fasihi
Fasihi; ni sanaa ya lugha inayoshughulikia masuala yanayomhusu binadamu matatizo yake, ndoto zake, matumaini yake, migogoro yake na jinsi anavyoingiliana na mazingira yake. (Wamitila, 2004).
Fasili hii imejaribu kufafanua vizuri kile ambacho fasihi inajihusisha nacho, kimsingi fasihi inajihusisha na wanadamu. Vitu vya msingi tunavyoviona katika fasili hii ni kwamba fasihi ni sanaa, na fasihi inatumia lugha lakini zaidi fasihi inajihusisha na wanadamu.
Dhima za Fasihi katika Jamii
Fafanua dhima za fasihi katika jamii
Dhima za fasihi katika jamii ni pamoja na hizi zifuatazo:
  • Kuburudisha jamii:Pamoja na mambo mengine fasihi inalenga kuburudisha jamii. Kupitia takribani vipera vyake vyote, fasihi huwa na kusudi la kufurahisha, kutumbuiza na kusisimua hadhira, kwa mfano kupitia nyimbo, hadithi, mashairi na kadhalika.
  • Kuelimisha. Fasihi hutumika kama nyenzo ya kuelimisha jamii, kupitia fasihi wanajamii wanaweza kuelimishwa juu ya mambo mabalimbali, kama vile juu ya umuhimu wa kuishi kwa amani, umuhimu wa kijikomboa kifikra, umuhimu wa kujikomboa kiuchumi, ubaya wa ufisadi na kadhalika.
  • Kuonya jamii. Fasihi ina jukumu la kuhakikisha wanajamii wanakaa katika mstari wa maadili ya jamii husika. Kupitia fasihi wanajamii wanapewa mwongozo wa jinsi ya kufuata mwelekeo unaokubalika katika jamii.
  • Kuunganisha jamii. Fasihi huleta watu katika jamii. Watu huunganishwa kupitia kazi mbalimbali za kifasihi, kwa mfano, kupitia nyimbo, miviga, vichekesho na kadhalika.
  • Kukuza lugha.Fasihi hutumia lugha kufikisha ujumbe wake katika jamii, lugha ya fasihi huwa ni ya kisanaa zaidi na hivyo kuifanya iwe yenye mvuto kwa wasikilizaji au wasomaji. Mtu anaposoma au kusikiliza kazi ya fasihi anapata ujuzi wa lugha. Lakini pia fasihi yenyewe inaweza kutumika kama chombo cha kukuza lugha. Wasimulizi na waandishi wa fasihi huhitaji kuwa na utajiri mkubwa wa lugha.
  • Kuhifadhi mila, tamaduni na itikadi za jamii. Kupitia fasihi simulizi, tamaduni na mila za jamii husika huhifadhiwa. Kwa mfano kupitia methali, misemo, nahau na vitendawili unaweza kujua mila na tamaduni za jamii husika.
  • Kukuza uwezo wa kufikiri. Vipera vingi vya fasihi huwachochea hadhira kufikiri sana ili kupata suluhisho. Kwa mfano, vitendawili, ngano za mtanziko na kadhalika.

Kuna tanzu mbili za fasihi, ambazo ni fasihi andishi na fasihi simulizi.
Dhana ya Fasihi Simulizi
Fafanua dhana ya fasihi simulizi
Fasihi Simulizi ni utanzu wa fasihi ambao unawakilisha sanaa ya lugha inayopitishwa kutoka kwa kizazi hadi kizazi kwa njia ya maneno/masimulizi ya mdomo.
Sifa na Dhima za Fasihi Simulizi
Elezea sifa na dhima za fasihi simulizi
Sifa za Fasihi Simulizi
  • Hupitishwa kwa njia ya mdomo
  • Ufanisi wa sanaa katika fasihi simulizi hutegemea uwezo wa msimulizi, au wahusika.
  • Masimulizi yake yanaweza kuathiriwa na mazingira, hisia na hali
  • Ni mali ya jamii. Hakuna mtu fulani anayemiliki sanaa katika fasihi simulizi.
  • Inaweza kubadilika kutoka kizazi hadi kizazi, au mazingira mbalimbali kwa sababu hutegemea kumbukumbu ya msimulizi.
  • Aghalabu huwa na funzo fulan
Dhima za Fasihi Simulizi
  • Kuburudisha - Hufurahisha na kuchangamsha hadhira
  • Kunasihi- kutolea mawaidha na kuonyesha mwelekeo unaotarajiwa katika jamii.
  • Kuelimisha watu kuhusu vitu mbalimbali hasa mazingira yao
  • Kutambulisha jamii - jamii mbalimbali husifika kutokana na sanaa zao katika fasihi simulizi kama vile nyimbo.
  • Kuhifadhi na kudumisha utamaduni wa jamii
  • Kuunganisha watu - huleta watu pamoja
  • Kukuza lugha - fasihi huimarisha lugha kwa kuwa hutumia mbinu mbalimbali za lugha.
  • Kuliwaza - hutoa huzuni na kuleta matumaini.
  • Kupitisha muda - wakati mwingine fasihi simulizi hutumika kupitisha muda.
  • Fasihi simulizi ni chombo cha mawasiliano hususani kupitia ngomezi.
Dhana ya Fasihi Andishi
Fafanua dhana ya fasihi andishi
Fasihi Andishi ni aina ya sanaa ambayo hutumia maneno ya maandishi kupitisha ujumbe kwa hadhira.
Kuna tanzu kuu nne za Fasihi Andishi:
  1. Hadithi Fupi – Hii ni kazi ya fasihi andishi yenye kisa kimoja na mhusika mkuu mmoja na maudhui yake sio changamani.
  2. Riwaya –Ni kazi ya fasihi andishi yenye wahusika wengi na muundo changamani ni ndefu na maudhui yake ni mapana.
  3. Tamthilia- ni kazi ya kisanaa yenye muundo wa kiugizikaji inayowasilishwa katika maandishi.
  4. Mashairi - mashairi yakiwa yamechapishwa pia hutambulika kama fasihi andishi.
Sifa na Dhima za Fasihi Andishi
Elezea sifa na dhima za fasihi andishi
Sifa za Fasihi Andishi
  • Hupitishwa kwa njia ya maandishi
  • Ni mali ya mtu binafsi
  • Haiwezi kubadilishwa papo kwa papo
  • Hutumia mbinu za lugha na mbinu za sanaa katika uwasilishaji wake.
Dhima za Fasihi Andishi
  • Kukuza lugha
  • Kuhifadhi kazi ya sanaa katika maandishi
  • Kuburudisha
  • Kuelimisha
  • Kukashifu tabia zisizoandamana na maadili ya jamii
  • Kuonya, kuelekeza, kunasihi
Tofauti kati ya Fasihi Simulizi na Fasihi Andishi
Onesha tofauti kati ya fasihi andishi na fasihi simulizi
Zifuatazo ni tofauti kati ya Fasihi Simulizi na Fasihi Andishi kama zilivyobainishwa katika jedwali hapa chini:
FASIHI SIMULIZIFASIHI ANDISHI
1.Huwasilishwa kwa njia ya mdomo na/au matendo.Huwasilishwa kwa njia ya maandishi
2.Ni mali ya jamii.Kazi andishi ni mali ya mwandishi (na mchapishaji)
3.Msimulizi anaweza kubadilisha sehemu FulaniKitabu kilichoandikwa hakiwezi kubadilishwa
4.Huhifadhiwa akiliniHuhifadhiwa vitabuni
5.Kazi simulizi hubadilika na wakatiKazi andishi haibadiliki na wakati
6.Huhitaji msimulizi na hadhira yake wawe mahali pamoja wakati wa masimuliziMsomaji anaweza kusoma kitabu cha hadithi peke yake, mahali popote, wakati wowote
7.Mtu yeyote anaweza kutunga na kusimuliaNi lazima mwandishi na msomaji wawe na uwezo wa kusoma
8.Hutumia wahusika changamano (wanyama, watu, mazimwi n.k)

Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

DHANA YA USHAIRI ILIVYOFAFANULIWA NA WATAALAMU MBALIMBALI

Ushairi kama moja kati ya tanzu za fasihi inayowasilishwa katika namna zote aidha kwa lugha ya maandishi au kwa lugha ya masimulizi una mchango au nafasi kubwa sana katika kunufaisha au kustawisha maisha ya binadamu kwa kumuelimisha, kumsisimua, kutunza na kuhifadhi amali zake pamoja na kukuza na kuendeleza lugha yake kama moja kati ya vipengere muhimu maishani mwake. Ushairi kama nudhumu katika fasihi simulizi hujumuisha nyimbo, ngonjera, tenzi na mashairi yenyewe. Ushairi wa Kiswahili waweza kuainishwa katika tanzu au katika kumbo mbalimbli kama asemavyo Mulokozi (1996) kuwa zipo kumbo kuu tatu ambazo ni ushairi wa kijadi au kimapokeo, ushairi wa mlegezo au huru na ushairi wa maigizo. Wanazuoni wafuatao wa mashairi ya kimapokeo wametoa maana za ushairi kama ifuatavyo:- Shaaban Robert (1958:37). “Ushairi ni sanaa inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi. Zaidi ya kuwa na sanaa ya vina, ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari…, mawazo, maoni na fikra za ndani zi...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...