Skip to main content

SHAIRI: MIE KUWA MWANAMKE


MIE KUWA MWANAMKE
Ni fahari na heshima,shukrani kwa muumba,
Najivunia daima,sitozijali kasumba,
Tangu zama za ujima,mama nguzo ya nyumba,
Mie kuwa mwanamke, ni thawabu kubwa sana.


Timamu hata kilema,ninayo kubwa thamani,
Nilizaliwa na mema,na pendo kubwa moyoni,
Mgonjwa na siha njema,bado ninayo amani,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Nazaliwa kuwa mama,mlezi aliye bora,
Niwe mwana mkulima,tajiri ama fukara,
Daima nitasimama,sitotishwa na bakora,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Zimepita nyingi zama,zenye mila za karaha,
Siwezi waza kuhama,kuitafuta furaha,
Nitatumia hekima,hadi kuipata raha,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Mila ziletazo homa,ni vyema kuzikomesha,
Kama italetwa ngoma,iwe siyo ya kukesha,
Pia nataka kusoma,na wanetu kusomesha,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Sitaki kuwaza nyuma,nyakati zilizoliza,
Tuliponyimwa kusema,kigoli hata ajuza,
Pia tuliachwa nyuma,marufuku kuongoza,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Mwana akiwa na homa,mama wa kwanza kujua,
Akihitaji huduma,mama atamuambia,
Mwanzo na mwisho wa juma,mama amuangalia,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Sasa mama asimama,kuwaongoza wengine,
Pia anafanya hima,awahi kazi nyingine,
Si kusoma si kulima,hafanyi ili mumwone,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Siri ya nyumba ni mama,mle ama mkalale njaa,
Anayo ile huruma,hadi baba ashangaa,
Kiazi atakichoma,mle akigaagaa,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Mama mama mama mama,jina tamu kwa mtoto.
Hata mbu akimwuma,tadhani kachomwa moto,
Dole mwiba ukichoma,utasikia muito,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Maziwa kapewa mama,na uchungu maksudi,
Kapewa nyingi dhima,mama kapewa juhudi,
Kumsifu sitokoma,kumweshimu sina budi,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Nikome hapa kwa leo,kujivuna kuwa mama,
Kwenu mama wa kileo,tunzeni hadhi ya mama,
Mama ninakupa vyeo,najivuna kuwa mama,
Mie kuwa mwanamke,ni thawabu kubwa sana.

Comments

Popular posts from this blog

DHANA YA USHAIRI ILIVYOFAFANULIWA NA WATAALAMU MBALIMBALI

Ushairi kama moja kati ya tanzu za fasihi inayowasilishwa katika namna zote aidha kwa lugha ya maandishi au kwa lugha ya masimulizi una mchango au nafasi kubwa sana katika kunufaisha au kustawisha maisha ya binadamu kwa kumuelimisha, kumsisimua, kutunza na kuhifadhi amali zake pamoja na kukuza na kuendeleza lugha yake kama moja kati ya vipengere muhimu maishani mwake. Ushairi kama nudhumu katika fasihi simulizi hujumuisha nyimbo, ngonjera, tenzi na mashairi yenyewe. Ushairi wa Kiswahili waweza kuainishwa katika tanzu au katika kumbo mbalimbli kama asemavyo Mulokozi (1996) kuwa zipo kumbo kuu tatu ambazo ni ushairi wa kijadi au kimapokeo, ushairi wa mlegezo au huru na ushairi wa maigizo. Wanazuoni wafuatao wa mashairi ya kimapokeo wametoa maana za ushairi kama ifuatavyo:- Shaaban Robert (1958:37). “Ushairi ni sanaa inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi. Zaidi ya kuwa na sanaa ya vina, ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari…, mawazo, maoni na fikra za ndani zi...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...