Skip to main content

SHAIRI: NAJUA NIPO SALAMA



Mama asante sana,pole kwa magumu yote,
Ninajua twafanana,kuliko viumbe vyote,
Siwazi tutagombana,ukinifanya vyovyote,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Najua umeteseka,kuumwa na kutapika,
Pia ulisonononeka,pia ulisikitika,
Moyoni ukaniweka,mama hukutikisika,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Marafiki ulikosa,wengi walipukutika,
Waliona kama kosa,wala hukusikitika,
Na hukufikiri posa,huruma ulijivika,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Bibi alinung'unika,kuona mama walia,
Uoga hukujivika,kweli ulivumilia,
Hujafa hujaumbika,moyo uliuambia,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Mwili ulipukutika,afya ikanyong'onyea,
Uoga ukafunika,huku ukiniombea,
Chakula hakikulika,mama ukanitetea,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Niliihisi faraja,ulipokuwa na baba,
Lilibomoka daraja,hukupunguza mahaba,
Nikawaza mama naja,wapi yupo wangu baba,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Ile sauti ya baba,ilinifanya niruke,
Nami nampenda baba,nilitamani nishuke,
Anayo hekima baba,daima umkumbuke,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Siku ile ninashuka,uliteseka mamangu,
Chakula hukukumbuka,hata ugali nachangu,
Neno lile nakumbuka,karibu sana mwanangu,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Usichoke usumbufu,na huku kulialia,
Kilio ni maarufu,pakiuma nitalia,
Utacheka maradufu,kiona nimetulia,
Nipo mikono salama,asante mama mpenzi.

Yapo mengi ya kusema,ila nakomea hapa,
Nimesharibu mama,mama usijenichapa,
Nibadili nguo mama,nzi wanifuata hapa,
Asante mama mpenzi,nipo mikono salama.

Nakupa ahadi mama,nitakuwa mama bora,
Sitokudharau mama,hata nipigwe bakora,
Daima nitasimama,nije kuwa mke bora,

Asante mama mpenzi,nitakupenda milele.

Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

KISWAHILI FORM 1: FASIHI SIMULIZI

KISWAHILI Form 1 Topic 4 FASIHI SIMULIZI Fasihi simulizi ni moja kati ya tanzu za fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo. Katika mada hii utajifunza na kisha utaweza kubainisha tanzu na vipera vya fasihi simulizi pamoja na ufafanuzi wake. Na pia utaweza kutofautisha kati ya kipera na kipera au kati ya utanzu na utanzu. Ubainishaji wa Tanzu za Fasihi Simulizi Tanzu za Fasihi Simulizi Bainisha tanzu za fasihi simulizi Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili. Tanzu za Fasihi Simulizi ni pamoja na hizi zifuatazo: Masimulizi/hadithi Semi Ushairi Mazungumzo Maigizo Ngomezi Ufafanuzi wa Vipera vya Tanzu za Fasihi Simulizi Vipera vya Hadithi Fafanua vipera vya hadithi SIMULIZI/ HADITHI Masimulizi ni fasihi yenye kusimulia habari fulan...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...