Skip to main content

SHAIRI: MWANANGU NGAO

Mwanangu leta mkeka, utandike upenuni,
Najua unanicheka, kujanika juani,
Sijali naneemeka, na wewe ukae chini,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.


Mwanangu kuna magumu, ya kusemwa na kutendwa,
Nusu tuzilambe sumu, kukufanya ukalindwa,
Tukakubali hukumu, ili usije kupondwa,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Ile aibu ya mwaka, aliyoileta dadako,
Mioyo ikatuwaka, alipoumwa kakako,
Mamako anazeeka, kisa kero za babako,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Shule wafukuzwa ada, madeni huku na kule,
Twachekwa sie wa shida, kufanya mwanetu ule,
Huku na huko ni mada,tunanyoshewa vidole,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Siku nimekengeuka, namnyanyasa mamako,
Mamako hakugeuka, kaficha kulinda jiko,
Na nyumba haikubomoka, akailinda miiko,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Mishale ilituchoma, na miiba kututesa,
Na wala hatukukoma, na hatukomi sasa,
Twasema mwanangu soma, ‘siharakie usasa,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Hatuoneshi makovu, ama kuzinena shida,
Muhimu kwepa maovu, na uishike ibada,
Usijezitaka mbivu, kabla ya kufika muda,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Nilimsumbua mama, nilivyokuwa mtoto,
Nilimwona kasimama, mie damu ya moto,
Na leo inaniuma, sikuwa mwema mtoto,
Mwanangu mzazi ngao, kaficha makovu mengi.

Yauma sikuwa bora, kuigundua huzuni,
Sikuziona busara, nikaziweka kichwani,
Nikaivuna hasara, mama ninamtamani,
Mwanangu mzazi ngao, anayo makovu mengi.

Nakuona wasinzia, na kijua chanichosha,
Sijui yamekwingia, ama ndio nakuchosha,
Wanao ‘tasimulia, na wao utawachosha,
Mama kapika viazi, vipi wawaza mikate?

Comments

Popular posts from this blog

NOTES ZA USHAIRI

USHAIRI     NI    NINI ? Shaaban Robert katika uandishi wa ushairi ameandika Tenzi na mashairi ya kimapokeo. Tenzi : Ni aina ya mashairi ya kimapokeo wenye sifa zifuatazo: Kimaudhui ; Ni utungo wenye maudhui yanayosimulia kwa urefu tukio fulani maalum. Waweza kuwa wasifu wa mtu au jambo la kihistoria. Mfano; S. Robert ameandika utenzi wa vita vya Uhuru, ameeleza kuhusu historia. Pia katika Mapenzi Bora, ameeleza kuhusu sifa za mapenzi bora. Utenzi ni utungo wa pili kati tungo za ushairi zenye beti nyingi. Utungo wa kwanza unaoongoza kuwa na beti nyingi kuliko zote katika ushairi ni Tendi. Lakini hapa tutaangazia tenzi zaidi. Utenzi hauna mizani nyingi aghalabu mizani nane, hauna mshororo bali una nusu mshororo/kipande mstari. Vilevile katika utenzi kipande mstari hakigawiki. Pia katika kipande mshororo kuna vipande vinne kwa kila ubeti. Mistari mitatu ya kwanza huwa na vina vyenye urari na kipande mstari cha mwisho/cha nne huwa...

Mpangilio wa sura katika utafiti

MADHARA YA MATUMIZI YA KARATASI ZA OMR KATIKA KUJIBIA MITIHANI. Na LEONARD RENATUS, 0759392855 Tasinifu hii ni kwa Ajili ya Kukamilisha Masharti ya  kukamilisha  Stashahada ya elimu ya msingi Chuo cha Ualimu Marangu. SURA YA KWAZA UTANGULIZI Utafiti huu umekusudia kuchunguza madhara na changamoto zitokanazo na karatasi za OMR  katika kujibia mitihani inayotolewa na baraza la matihani Tanzania (NECTA) . Katika sura hii utafiti huu utaangalia vipengele vifuatavyo:- Utangulizi. Usuli wa tatizo. Tamko la utafiti. Lengo kuu la utafiti. Malengo mahsusi yautafiti. Umuhimu wa utafiti. Mawanda ya utafiti. Tafsiri za istlahi zilizotumika 1.2    USULI WA TATIZO OMR ni kifupi cha maneno ya Optical Mark Reader ni mashine ambayo inatumika kusahihishia karatasi za wanafunzi waliofanya mitihani. Kwa hapa Tanzania karatasi hizi hutumika katika kujibia mitihani ya kumaliza elimu ya msingi kwa darasa la saba . Njia hii ya kusahihishia miti...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...