Skip to main content

SHAIRI: NILIPOKUWA MATEKA


Si wote waliojua,zaidi ya mtekaji,
Mwenyewe sikutambua,nikajisi mjuaji,
Wale walonililia,nikahisi wauaji,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Nilitenda atakavyo,aliyeniteka akili,
Nilipoambiwa sivyo,sikutaka kukubali,
Na nikawajibu ovyo,nikitusi kwa ukali,
Nilipokuwa mateka, niliwaumiza wengi.



Mwanangu na mama yake,walinililia kutwa,
Akakonda bibi yake,hofu ya mwana kuachwa,
Na mawazo yangu kwake,ni kama yalishafutwa,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Marafiki na babangu,waliniona wazimu,
Nilimsahau na Mungu,na sikuhofu kuzimu,
Nikapuuza uchungu,wa mama yangu muhimu,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mtesi nikamwamini,kila asemalo sawa,
Dada atasema nini,ni'shajiotesha mbawa,
Sijui cha ibadani,na pombe ikawa dawa,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Lile chozi la mamangu,mwanangu na mama yake,
Pia sauti ya Mungu,kupitia watu wake,
Imekuwa tiba kwangu,nipo huru mtu wake,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Nisamehe walimwengu,nisamehewe mbinguni,
Pole na kipenzi changu,unirejeshe moyoni,
Sasa naona uchungu,najua mateka nani,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mwanangu usinizile,pole kwa yote magumu,
Yasahau yote yale,zikutoke zote sumu,
Yameshapita ya kale,na wala usilaumu,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mama mkwe nakuomba,yasamehe yalopita,
Usimwambie mjomba,tayari nimeshajuta,
Mbuzi usije muomba,mwenyewe nitamleta,
Tutambike tule na tunywe,tufurahi tusahau.

''Kauli za Makabwela 2017''

Comments

Popular posts from this blog

DHANA YA USHAIRI ILIVYOFAFANULIWA NA WATAALAMU MBALIMBALI

Ushairi kama moja kati ya tanzu za fasihi inayowasilishwa katika namna zote aidha kwa lugha ya maandishi au kwa lugha ya masimulizi una mchango au nafasi kubwa sana katika kunufaisha au kustawisha maisha ya binadamu kwa kumuelimisha, kumsisimua, kutunza na kuhifadhi amali zake pamoja na kukuza na kuendeleza lugha yake kama moja kati ya vipengere muhimu maishani mwake. Ushairi kama nudhumu katika fasihi simulizi hujumuisha nyimbo, ngonjera, tenzi na mashairi yenyewe. Ushairi wa Kiswahili waweza kuainishwa katika tanzu au katika kumbo mbalimbli kama asemavyo Mulokozi (1996) kuwa zipo kumbo kuu tatu ambazo ni ushairi wa kijadi au kimapokeo, ushairi wa mlegezo au huru na ushairi wa maigizo. Wanazuoni wafuatao wa mashairi ya kimapokeo wametoa maana za ushairi kama ifuatavyo:- Shaaban Robert (1958:37). “Ushairi ni sanaa inayopambanuliwa kama nyimbo, mashairi na tenzi. Zaidi ya kuwa na sanaa ya vina, ushairi una ufasaha wa maneno machache au muhtasari…, mawazo, maoni na fikra za ndani zi...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...