Skip to main content

SHAIRI: NILIPOKUWA MATEKA


Si wote waliojua,zaidi ya mtekaji,
Mwenyewe sikutambua,nikajisi mjuaji,
Wale walonililia,nikahisi wauaji,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Nilitenda atakavyo,aliyeniteka akili,
Nilipoambiwa sivyo,sikutaka kukubali,
Na nikawajibu ovyo,nikitusi kwa ukali,
Nilipokuwa mateka, niliwaumiza wengi.



Mwanangu na mama yake,walinililia kutwa,
Akakonda bibi yake,hofu ya mwana kuachwa,
Na mawazo yangu kwake,ni kama yalishafutwa,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Marafiki na babangu,waliniona wazimu,
Nilimsahau na Mungu,na sikuhofu kuzimu,
Nikapuuza uchungu,wa mama yangu muhimu,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mtesi nikamwamini,kila asemalo sawa,
Dada atasema nini,ni'shajiotesha mbawa,
Sijui cha ibadani,na pombe ikawa dawa,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Lile chozi la mamangu,mwanangu na mama yake,
Pia sauti ya Mungu,kupitia watu wake,
Imekuwa tiba kwangu,nipo huru mtu wake,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Nisamehe walimwengu,nisamehewe mbinguni,
Pole na kipenzi changu,unirejeshe moyoni,
Sasa naona uchungu,najua mateka nani,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mwanangu usinizile,pole kwa yote magumu,
Yasahau yote yale,zikutoke zote sumu,
Yameshapita ya kale,na wala usilaumu,
Nilipokuwa mateka,niliwaumiza wengi.



Mama mkwe nakuomba,yasamehe yalopita,
Usimwambie mjomba,tayari nimeshajuta,
Mbuzi usije muomba,mwenyewe nitamleta,
Tutambike tule na tunywe,tufurahi tusahau.

''Kauli za Makabwela 2017''

Comments

Popular posts from this blog

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

NOTES ZA USHAIRI

USHAIRI     NI    NINI ? Shaaban Robert katika uandishi wa ushairi ameandika Tenzi na mashairi ya kimapokeo. Tenzi : Ni aina ya mashairi ya kimapokeo wenye sifa zifuatazo: Kimaudhui ; Ni utungo wenye maudhui yanayosimulia kwa urefu tukio fulani maalum. Waweza kuwa wasifu wa mtu au jambo la kihistoria. Mfano; S. Robert ameandika utenzi wa vita vya Uhuru, ameeleza kuhusu historia. Pia katika Mapenzi Bora, ameeleza kuhusu sifa za mapenzi bora. Utenzi ni utungo wa pili kati tungo za ushairi zenye beti nyingi. Utungo wa kwanza unaoongoza kuwa na beti nyingi kuliko zote katika ushairi ni Tendi. Lakini hapa tutaangazia tenzi zaidi. Utenzi hauna mizani nyingi aghalabu mizani nane, hauna mshororo bali una nusu mshororo/kipande mstari. Vilevile katika utenzi kipande mstari hakigawiki. Pia katika kipande mshororo kuna vipande vinne kwa kila ubeti. Mistari mitatu ya kwanza huwa na vina vyenye urari na kipande mstari cha mwisho/cha nne huwa...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...