ZANA ZA KUFUNDISHIA

 ZANA ZA KUFUNDISHIA

1.  Zana za kufundishia, ni kitu au vitu vyovyote vinavyojengwa na kutumika katika kuinua kiwango cha elimu. Mwalimu yeyote anapaswa kujifunza utengenezaji na matumizi ya zana kwani ni nyenzo muhimu sana katika kazi ya kufundisha na kujifunza. Lengo hasa la kutumia zana katika kufundisha ni kukuza na kuinua kiwango cha kujifunza cha mwanafunzi. Kikawaida zana za kufundishia na kujifunzia hupaswa kuwa na sifa kama vile kubebeka, kuonekana, kuhifadhika, kusadifu mada, iendane na mazingira na iendane na umri wa wanafunzi. Baadhi ya waandishi wamebainisha aina tano za zana kama vile vitu halisi, bandia, video na sinema, chati na picha, redio, santuli, tepu rekoda.
Zifuatazo ni aina kuu tatu  za zana za kufundishia katika ngazi za elimu yaani elimu ya msingi, sekondari, na sekondari ya juu:-
Zana za kuonekana, hizi ni zana ambazo mwalimu huzitoa katika mazingira halisi ambapo huziandaa yeye mwenyewe au kuwaagiza wanafunzi waziandae ili kuweza kufanikisha suala zima la ujifunzaji. Mfano wa zana hizi ni kama vile majani ya miti, mawe, na nyingine nyingi. Mwalimu huweza kutumia zana kama vile mawe wakati wa ufundishaji wa hesabu za kujumlisha, kutoa, kuzidisha, na hata kugawanya.
Zana za kusikika, zana hizi ni zana zinazotoa sauti kama vile redio, kinanda, ngoma. Zana hizi humsaidia mwalimu katika tathimini ya kujua wanafunzi wenye matatizo ya kusikia na pia humsaidia mwalimu kufanikisha ufundishaji wake kwa wanafunzi wake hasa katika mada inayohusiana na usikivu.
Zana za kusikika na kuonekana, zana hizi ni zana ambazo huweza kutoa sauti na hata kutoa picha. Zana hizi ni kama vile runinga na tanakilishi. Zana hizi huweza kumsaidia mwalimu katika ufundishaji wake, ambapo mwalimu huwaongoza wanafunzi kujifunza somo fulani kwa kutazama picha na kusikiliza sauti itolewayo katika runinga, tanakilishi au simu. Hivyo zana hizi ni muhimu sana katika suala au mchakato mzima wa ufundishaji na ujifunzaji kwa sababu haibagui wanafunzi kutokana na hali zao, mfano wasoona au wasosikia.
Baada ya kuangalia aina tofauti tofauti za zana, hebu tuangalie faida ya zana za kufundushia. Zipo faida nyingi za zana za kufundishia lakini hizi hapa chini ni baadhi tu:-
Hujenga ubunifu, matumizi ya zana za kufundishia huweza kujenga ubunifu kwa mwanafunzi na pia hata kwa mwalimu kwani uundaji wa zana huitaji maarifa ya ziada ili kuikamilisha. Mwanafunzi huweza kuwa mbunifu pindi tu atakapo agizwa na mwalimu kutengeneza zana, kama vile kufuma kitambaa, kuchora picha na kadharika.
Humjengea mwanafunzi kumbukumbu ya kudumu, mwanafunzi atakapofundishwa kwa kutumia zana mbalimbali kama vile tufe kama mfano wa umbo la dunia. Mwanafunzi huweza kuweka kumbukumbu kwa mda mrefu kwa sababu kujifunza kwa kuona kitu husika humjengea mwanafunzi uwezo wa kukumbuka tofauti na kujifunza bila kuona kitu husika. Hivyo utumiaji wa zana katika ujifunzaji ni muhimu sana kwa sababu hufanya somo kueleweka kwa urahisi.
Hujenga udadisi, ujifunzaji kwa kutumia zana una faida kwa kuwa hujenga udadisi kwa mwalimu na mwanafunzi. Hii hutokea pale mwanafunzi anapodadisi kwa undani zaidi namna au jinsi kitu kilivyoundwa mfano wa zana kama vile redio, runinga na zana zingine. Hivyo zana zina umuhimu sana katika ujifunzaji na ufundishaji.
Kurahisisha tendo kufundisha na kujifunza, utumiaji wa zana hurahisisha suala zima la ujifunzaji na kufundisha. Wanafunzi huelewa zaidi pale wanapoona kitu halisi hivyo hufanya somo liwe zuri kwa wanafunzi na waweze kulifurahia. Hii humfanya mwanafunzi aweze kuelewa kwa urahisi zaidi kuliko pale anapojifunza kwa kufikiri tu pasipo kuona kitu kinachozungumziwa.
Wanafunzi wengi hushiriki, katika ujifunzaji wa kutumia zana wanafunzi wengi huwepo katika somo kwa sababu, wanafunzi hupendelea zaidi kujifunza kwa kuona kitu halisia kinachosemwa na mwalimu wa somo. Mfano wakati wa kufundisha kompyuta, wanafunzi wengi huudhulia endapo kompyuta itakuepo kama zana ya kufundishia, kwani wanafunzi wataona kipanya, chombo chenye vibonyezo, kompyuta yenyewe, na kioo cha kompyuta.
Mwanafunzi hachoki kujifunza, katika ujifunzaji wa kutumia zana mwanafunzi hachoki kujifunza kwani hushiriki papo hapo katika suala zima la ujifunzaji.  Mwanafunzi hutamani mwalimu aendelee kufundisha, kwa kuwa vitu vinavyofundisha ni vitu ambavyo mwanfunzi huviona kwa macho yake mfano kuwaonesha wanafunzi filamu ya riwaya ya mfadhili.  Hivyo mwanafunzi hachoki kujifunza.
Kuna mambo mbalimbali ya kuzingatia wakati wa kuandaa zana za kufundishia, mambo hayo ni kama vile ukubwa wa zana, idadi ya wanafunzi, maudhui yaendane na zana, uwezo wa mwalimu katika kuelezea mada.
Kuna namna tofauti tofauti za kuandaa zana za kufindishia lakini zifuatazo ni baadhi tu ya namna ya kuandaa zana za kufundishia nazo ni:-
Kuchonga, hii ni ile namna ya kuandaa zana kwa kutumia miti kama malighafi. Mwalimu hutumia miti kama malighafi ya kuchongea zana kama vile kinyago, kuchonga rula, na vifaa vingine vinavyotokana na malighafi miti. Zana za kuchonga hupelekea mwanafunzi kuwa mdadisi katika kuandaa zana hizo, kwa kuwa hutumia maarifa mengi katika uandaaji wake.
Kuchora, namna hii ya kuandaa zana za kufundishia, ni namna inayohusisha matumizi ya kalamu ya mkaa, rangi za aina mbalimbali, manila, na vifaa vingine. Hapa mwalimu huweza kuandaa zana kama vile ramani, picha ya baadhi ya wanyama, alfabeti, namba, maumbo mbalimbali kama vile pembe tatu, mstatili, mraba na maumbo mengine mengi.
Kufinyanga, hii ni namna ya uandaaji wa zana kwa kutumia udongo kama malighafi ya kutengenezea zana za kufundishia. Mwalimu huchanganya udongo na maji ili kuweza kutengeneza zana kama vile vyungu, sahani, kinyago na kadharika. Mwalimu anaweza kuwashirikisha wanafunzi katika utengenezaji wa zana hizi ili kufanikisha somo la stadi za kazi.
Kukusanya, hii ni namna ya kuandaa zana kwa kutafuta vifaa vya kujifunzia na kifundishia yaani zana kwa kuzikusanya kutoka katika mazingira halisi. Tendo hili laweza kutendeka kwa kuwaagiza wanafunzi au mwalimu mwenyewe kuziokota, kununua au kuchukua kutoka nyumbani kwake. Zana hizo kama machungwa, vijiko, na hata redio. Zana hizi humsaidia mwalimu katika kufanikisha suala zima la ufundishaji kwa wanafunzi wake.
Kufaragua, hii ni namna ya kuandaa zana kwa kutumia vifaa au makunzi yasio halisi na yanayopatikana katika mazingira husika. Ufaraguzi unaweza kluwa wa namna mbalimbali kama vile kutumia kitu papo kwa papo kinyume na matumizi yake ya kawaida, unapotumia kalamu ya mkaa kama kishikizi katika kupiga mstari (hapa utakua umetumia kalamu ya mkaa kama rula). Au kutumia mpira kama tufe katika kufundisha kuwa dunia ni duara.
Kufuma, hii ni namna ya kuandaa zana kwa kutumia nyuzi za rangi mbalimbali kutengeneza zana kama vile vitambaa, sweta pamoja na zana zingine zinazotokana na malighafi nyuzi. Mwalimu huweza kuwaagiza wanafunzi walete nyuzi ili kuweza kuziandaa zana hizo katika mazingira ya shule ili aweze kutambua wanafunzi waliomuelewa wakati anafundisha darasani. Hii ni nzuri kuliko mwalimu akiwaagiza wanafunzi wake watengenezee nyumbani.
Kwa ujumla,  katika mchakato wa ufundishaji na ujifunzaji zana sio lazima vitu au vifaa, kwa sababu kila kitu kinachoshikika endapo kitakuwa na mchango wowote katika kufanikisha suala zima la ufundishaji na ujifunzaji kitu hicho kitakua ni zana. Hivyo mwalimu na wanafunzi pia huweza kuwa zana pindi wawapo darasani kwa ajili ya somo mahususi.

Comments

  1. Ni somo zuri sana tna linaegemea kwenye ufundiahaji wa kiswahili kwa wageni.... Heko

    ReplyDelete
  2. Aisee nukuuu hizi ziko vizuri sana katika suala la ufundishaji na ujifunzaji kwa mwanafunzi,zitakazo wezesha tendo la urithishaji wa maarifa,ujuzi,stadi,mitazamo,mienendo na mielekeo toka kizazi hadi kizazi.

    big up sana,

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

NOTES ZA USHAIRI

MBINU ZA KUFUNDISHIA

DHANA YA USHAIRI ILIVYOFAFANULIWA NA WATAALAMU MBALIMBALI