Skip to main content

TAHAKIKI YA RIWAYA YA KUSADIKIKA


UTANGULIZI 

Katika kujadili vipengele mbalimbali vya Fani na maudhui vilivyotumiwa katika riwaya ya kusadikika iliyoandika na Shaaban Robert Washiriki hatukujikita zaidi katika kujadili maana ya riwaya za wataalamu mbalimbali bali tuliweza kujadili kazi hii kwa kuchambua vipengele vya fani na maudhui kutokana na masimulizi ya nchi ya Kusadikika. 

Masimulizi ya kitabu kwa kifupi. 

Riwaya ya kusadikika ni kitabu kinachoelezea masimulizi ya nchi ya kusadikika ambayo mwandishi ameanza kwa kusimulia tukio la kushitakiwa kwa Karama ambaye ndiye Mhusika mkuu kwa tuhuma za kuihujumu serikali ya Kusadikika. Kwa maelezo ya Waziri Majivuno aliwasilisha mashitaka haya mbele ya Mahakama eti kwa sababu Karama alikuwa akitoa elimu ya sheria ambayo kwa Mtazamo wa Waziri huyu alidai kuwa angewafanya raia wa kusadikika kuelewa haki zao ambako kungepelekea wananchi hao kutotii serikali au kwa namna nyingine kungekomesha unyanyasasaji, uonevu na uongozi mbaya wa watawala wa kusadikika na hivyo waziri Majivuno alijawa hofu kubwa sana. 


Riwaya imeendelea kusimulia namna mshitakiwa Karama alivyowasilisha utetezi wake mbele ya Mahakama ya Kusadikika iliyoundwa na Mfalme na Madiwani. Karama aliwasilisha utetezi huo kwa kuthibitisha jinsi serikali ilivyoshindwa kuthamini michango mbalimbali ya wananchi wake kwa kuelezea historia wajumbe mbalimbali waliojitoa kwenda kufanya utafiti wa namna ya kuendeleleza nchi yao. Masimulizi yake yaliwataja hasa wajumbe 6 waliotumwa mipakani au pande zote 6 ambazo nchi ya kusadikika inapakana nayo. Pande hizo ni Kaskazini, Mashariki, Kusini, Magharibi, Mbinguni na Ardhini. Hatima ya wajumbe hawa ambao walikuwa wazalendo waliishia Kifungoni pindi waliporejea kutoka walikotumwa. 

Mwisho wa riwaya hii mwandishi anaelezea hukumu ya Karama ambapo Mahakama iliyoongozwa na Mfalme ilivyomtoa hatia mtuhumiwa kwa kauli moja ya kuwa hana hatia na Mfalme kuagiza wajumbe wote waliokuwa wanatumikia kifungo kufunguliwa na kulipwa fidia kwa kunyanyaswa pamoja na jitihada zao. 

Baada ya muhtasari wa masimulizi ya nchi ya kusadikika tuliweza kujadili vipengele vinavyounda Fani na Maudhui ya kazi ya riwaya ya kusadikika kama ifuatavyo;- 

Fani ni ujuzi au Mbinu mbalimbali azitumiazo msanii kuwasilisha ujumbe au Fikra zake kwa hadhira aliyoikusudia. Fani inaundwa na vipengele vya Mandhari, Wahusika, muundo, Mtindo na Matumizi ya lugha. 

Maudhui ni jumla ya mawazo yanayowasilishwa na msanii wa kazi ya kifasihi katika kazi yake. Maudhui huundwa na vipengele vya Dhamira, Ujumbe, Falsafa, Migogoro, Mtazamo na Msimamo. 

Uchambuzi wa Vipengele mbalimbali alivyovitumia mwandishi wa riwaya hii ya Kusadikika ni: 

Mandhari: ambayo humaanisha mahali au sehemu ambayo tukio linafananyika. Mwandishi ametumia mandhari ya Kufikirika ambayo haiwezi kujidhihirisha kwa macho ya kawaida (haionekani) kwani ni nchi inayoelea angani. Pia ametumia mji wa sadiki na mipaka au pande sita zinazopakana na nchi hii za Kaskazini, Mashariki, Kusini, Magharibi, Ardhini na Mbinguni. 

Wahusika ni mtu au watu, wanyama, na mimea anaotumia mwandishi katika kuwasilisha kazi yake kwa hadhira iliyokusudiwa. Kwa kiasi kikubwa Mwandishi ametumia Wahusika ambao aliowapa majina yanayosawiri tabia zao na wahusika ambao hawabadiliki badiliki ;- 

Karama, Huyu ni mhusika mkuu ambaye pia alikuwa Jasiri na Shujaa, Mwanasheria, Mzalendo mtetezi wa haki na Mshitakiwa. Vilevile mhusika huyu alichorwa mwema kuanzia mwanzo hadi mwisho. 

Majivuno, Waziri wa kusadikika, mwenye uchu wa madaraka, mwenye haiba, asiye na uzalendo, kiongozi anayelindwa na Mfalme na asiye na shukurani. 

Mfalme, Kiongozi wa kusadikika, Katili, Mjinga, mwenye tama ya uongozi, mkuu wa baraza la Mahakama. 

Madiwani, Wasaliti, wakuu wa mahakama, waonevu, wakatili, wenye dhuluma na sio wazalendo. 

Mudir wa sheria, mwanasheria wa serikali, Mjinga, msaliti na asiye mzalendo. 

Buruhani, Mjumbe wa kaskazini, Jasiri, Mzalendo mpenda haki, Mwanaharakati, Mfungwa na maskini. Msanii anasema “Hii ilikuwa safari ya ujasiri iliyotaka uthabiti na matumaini, mwenye heshima, hodari na mwaminifu alitakiwa ajitolee mwenyewe kwa safari hii” uk.12. 

Fadhili, Mjumbe aliyetumwa mashariki, Jasiri, Mzalendo, mpenda haki, Mfungwa na maskini. “Mtu mwenye sifa njema alitakiwa kujitolea mwenyewe kwa ujumbe wa mashariki na mtu kama huyu alipatikana upesi sana kuliko ilivyokuwa ikitazamiwa” uk.16. 

Kabuli, Mjumbe wa kusini, jasiri, Mzalendo, Mpenda haki, Maskini na mfungwa. 

Auni, Mjumbe wa Magharibi, Jasiri, Mzalendo, Mpenda haki, Mwananchi wa kawaida na mfungwa. 

Sapa na Salihi, walikuwa vipofu, wananchi wa magharibi, Sapa alikuwa mwenye tama na wivu, Sapa alikuwa mpole, Sapa aliomba upofu. 

Radhaa, mjumbe wa mbinguni, Jasiri, mzalendo, mpenda haki, Mfungwa na Maskini. 

Amini, mjumbe wa ardhini, Jasiri, mpenda haki, mzalendo na mfungwa. 

Wahusika wengine ni wananchi, bwana Taadabuni, katibu wa serikali, bwana Komeni, Amiri jeshi, bwana fujo, mlinda hazina, bwana Baromini na wananchi wa pande zingine. 

Muundo, ni namna au jinsi mwandishi anavyopangilia visa na matukio katika kazi yake ya kifasihi. Mwandishi ametumia muundo wa moja kwa moja ambapo katika mpangilio wa masimulizi ameanza mwanzo wa kisa kwa kuonesha jinsi mashitaka yalivyowasilishwa, kukafuatiwa na utetezi wa mshitakiwa au kile mwandishi alichokiita maombezi mbele ya Mfalme na Madiwani kwa kusimulia historia ya kusadikika kupitia wajumbe sita waliotumwa pande sita na kuishia kifungoni kama sehemu ya pili ya kisa na hatimaye alimalizia kwa kuelezea hukumu ya kesi ya Karama ambapo Mfalme na Madiwani walionesha kuwa mtuhuma hakuwa na hatia na kufunguliwa kwa wajumbe sita na kuachiwa huru huku Mfalme akiamuru walipwe fidia. 

Mtindo. Ni namna mwandishi anavyoiumba kazi yake ya kifasihi. Mwandishi Shaaban Robert ametumia mitindo mbalimbali katika kazi hii ya riwaya ya kusadikika kama vile, ametumia maswali hasa katika sehemu ya mwisho ya kitabu, ametumia dayalojia kati ya Sapa na Salihi uk. 29, ametumia masimulizi kwa kiasi kikubwa katika kazi hii ambayo kwake ndio mbinu kuu pamoja na matumizi ya nafsi ya pili na tatu umoja na nafsi ya tatu wingi sehemu kubwa ya riwaya. 

Lugha. Mwandishi ametumia lugha ngumu ambayo si rahisi kueleweka kwa msomaji kutokana na kutumia misamiati isiyoeleweka. Hali hii ya kutumia lugha ngumu ililengwa kukwepa makucha ya wakoloni. Mfano wa misamiati hiyo ni sudusi, takirifu, kafaungo, hutasawari, akapatilizwa, ali, kujikagajuu, Kuyabisika, kujikaga, Kadura n.k. Pia mwandishi ametumia vipengele vya Tamathali za semi ambazo ni ;- 

Methali. Kitanda usichokilalia hujui Kunguni wake. 

Msiba wa kujitakia hauna kilio. Lila na fila hawatangamani. 

Misemo. 

Kumtosa mshitakiwa katika bahari ya maangamizi. 

Tashibiha. 

Umri wake mkubwa ulizofanya nywele zake za kichwani kuwa nyeupe kama fedha. 

Uso wa kipofu wa kwanza ulikuwa na furaha kama bwana harusi. 

Alikuwa na tabia ya kuficha siri kama kaburi lifunikalo maiti. 

Anamaneno kama kitabu 

Tashihisi. 

Giza limezalo nuru na ufupisho uoni wa macho. 

Wakati una mabawa kama ndege uk. 11. 

Jina la Kitabu (KUSADIKIKA). Jina la kitabu linasawiri yaliyomo katika riwaya hii kwani limetokana na neno “sadiki” likimaanisha “Amini” hivyo linaweza kusemwa kuwa ni kuaminika. Mwandishi anatuonesha kuwa Wasadikika ni wajinga kwani hawakujihusisha na uchambuzi wa masuala yake waliishia kuamini na kukubali kila jambo mwandishi anasema “Imani ya Kusadikika ni nguzo imara ya majengo ya utawala wa Wasadikika” wakati mataifa mengine yalipojifananisha kwa mambo kama vile enzi, uwezo na fahari nyingine taifa la kusadikika lilijivuna kwa sababu ya kusadiki mambo yaliyotoka vinywani mwa watu wake” uk. 4-5. 

Kwa washiriki wa uchambuzi huu wanakiri kuwa kwa kiasi kikubwa tumefanikiwa kuchambua haya katika vipengele vya fani na maudhui alivyotumia msanii Shaabani Robert katika riwaya ya Kusadikika ingawa si vyote vilivyotumika katika vipengele hivi tumeweza kuviainisha. (rejea masimulizi ya kitabu) 
KIPENGELE CHA MAUDHUI. 

Maudhui ni jumla ya mawazo aliyonayo msanii katika kazi yake ya kifasihi, Kipengele cha maudhui kinaundwa na ujumla, dhamira, migogoro, falsafa, Msimamo/Mtazamo. 
Dhamira mbalimbali 

Dhamira kuu ni Ukombozi: Dhamira hii ndio kuu katika riwaya ya kusadikika iliojikita kwenye ukombozi wa kifikra na ukombozi wa kisiasa. Mwandishi amemtumia mhusika karama aliyeanzisha elimu ya sheria yenye lengo la kuwezesha wananchi ili wawezekushiriki katika mambo mbalimbali ya nchi. 

Ukombozi wa kisiasa unarejelea harakati zilizoongozwa na Karama na wajumbe sita zenye lengo la kuleta mabadiliko katika nchi ya kusadikika kuhusu haki na uongozi (viongozi). Msanii anasema “Kwa nini wanasiasa wa kusadikika hawakuwaacha kama Karama kujishughulisha na mambo yaliyowapita vimo vyao” 

Matabaka. Hali ya wahusika kuwa na hadhi au makundi au madaraja tofauti tofauti. Katika riwaya ya kusadikika ameonesha matabaka ya namna mbalimbali kama;- 

Tabaka la viongozi na wananchi, matajiri na wasomi na wasio wasomi na wenye haki na wasio na haki. Katika kudhihirisha matabaka haya mwandishi ameeleza kwa mifano baadhi ya maeneo haya anasema “Sheria za wasadikika zilikuwa hazimuamuru mshitakiwa kujitetea juu ya ushahidi wa mshitaki. Aghalabu mashitaka mengi yalikubaliwa bila ya swali wala kiapo kama mashitaka yaliletwa mbele ya baraza na wafalme, watoto wao, matajiri au watu wengine maarufu nguvu ya desturi hii ilifanywa maradufu. Hapana shaka salama ya watu wadogo ilikuwa kidogo sana katika nchi ya kusadikika” uk.7. 


Uongozi Mbaya. Mwandishi amedhihirisha hili kwa kuwatumia wahusika waziri Majivuno, Wafalme, Madiwani na matajiri ambao ndio waliochorwa kwa taswira ya kuwa Wanahaki zaidi kuliko wananchi wa kawaida. Tunapozungumzia uongozi mbaya ni hali ya utawala kutowajali kwa kuwasaidia wananchi wa kawaida kisiasa, uchumi, na kijamii. 

“Aghalabu Mashitaka mengi yalikubaliwa bila ya swali wala kiapo kama mashitaka yaliletwa mbele ya baraza na wafalme, watoto wao, matajiri au watu wengine maarufu nguvu ya desturi hii ilifanywa maradufu” uk.7. 

Uzalendo na ujasiri. Uzalendo ni hali ya mtu kuipenda nchi yake na kujitoa kuipigania katika mambo mbalimbali yanayokwamisha maendeleo. Mwandishi anasema “pigano la kufa na kupona lilikuwa mbele yake” uk.8. “alikuwa hana silaha nyingine za kuokolea maisha ila zana hizi” uk.9. “Msema kweli hukimbiwa na marafiki zake, siwezi kuikana kweli kwa kuchelea upweke wa Kitambo nikajinyima ushirika wa milele unaotazamiwa kutokea baada ya kushindwa kwa uongo”uk.9. 

Mwandishi amewatumia wahusika Karama, Buruhani, Fadhili, Kabuli, Auni, Radhaa, Amini kuonesha ujasiri na uzalendo walijitoa na kufanyakazi katika masahibu mengi tena bila ya kukata tama huku baadhi wakiishia kifungoni. Hatimaye waliweza kushinda. Mwandishi anasema “kwa kazi zake bora na uaminifu mwingi hakushukuriwa bali kuvunjiwa kadiri, aliaibishwa kuwa alileta uzushi ulikuwa hauna faida katika nchi zaidi ya hayo alitumbukizwa katika kifungo cha maisha” 

Ujinga. Hali ya watu kutoelewa mambo mbalimbali ya msingi kijamii kisiasa, kiutamaduni na kiuchumi. Mfano haki sheria na uongozi nakadhalika. Shaaban Robert amethibitisha uwepo wa ujinga katika nchi ya kusadikika kupitia viongozi na wananchi waliosadiki mambo yao na kuyakana ya nje. Pia mwandishi amewatumia wananchi waliohudhuria mahakamani siku ya kwanza ya mashitaka. Msanii anasema “Baadhi ya watu wachache waliokuja barazani kusikiliza kesi hii walimsikitikia mshitakiwa wengi walikuwa wakinong’onezana kuwa msiba wa kujitakia hauna kilio” uk 7. “ujinga wao haukuyazuia maendeleo tu lakini hasa ulirudisha nchi nyuma vilevile” uk. 14. “Twaona kuwa mshitakiwa hana hatia ila alikuwa akitafuta jinsi ya kuisaidia sheria ya kusadikika kwa njia ngeni” Maelezo haya ni matokeo ya ufumbuzi wa ujinga uliokuwa umekithiri kwa viongozi wa kusadikika na wananchi wake. 

Uonevu na Ukandamizaji (kukosekana kwa haki). Hali ya kutothaminiwa, kupewa haki na kuhukumiwa bila ya kufanya kosa lolote, na wakati mwingine kutopewa nafasi ya umuhimu katika tabaka fulani la watu “sheria za kusadikika zilikuwa hazimuamuru mtu yeyote kujitetea juu ya ushahidi wa mshitaki” uk.7. Buruhani, Fadhili, Kabuli, Auni, Radhaa, Amini walifungwa tena kwa kunyanyaswa Mwandishi anasema “Natoa amri watu sita waliotajwa wafunguliwe mara moja, inasikitisha sana kwa dhuluma juu ya watu hawa hazikutengenezwa mpaka leo. Gereza ni makao ya wahalifu na watu hawa si wahalifu” Mhusika mkuu karama pia alishitakiwa na Waziri majivuno kwa hulka tu za ukandamizaji. 

Umaskini. Ni hali ya kutomudu kujipatia mahitaji mbalimbali ya kila siku kwa kiwango kinachoridhisha (cha kutosha) Mwandishi anasema “kwa kukosekana kwa Madaraja mito inafanya shida juu ya watu walio ng’ambo moja kukutana na Ng’ambo nyingine, maradhi hayajapata uuguzaji, vifo vya mapema hapa katika mwaka mmoja jumla yake yatisha kuliko ile ya vifo vitokeavyo katika nchi nyingine katika karne moja” Uk. 25. Pia “Aghalabu Mashitaka mengi yalikubaliwa bila ya swali wala kiapo kama mashitaka yaliletwa mbele ya baraza na wafalme, watoto wao, matajiri au watu wengine maarufu nguvu ya desturi hii ilifanywa maradufu. Hapana shaka salama ya watu wadogo ilikuwa kidogo sana katika nchi ya kusadikika” uk. 7. Maelezo haya yanaonesha uwezekano mkubwa wa uwepo wa kundi kubwa la watu masikini ambao ndio walioguswa na sheria za kusadikika. 

Dhamira nyingine ndogondogo zilizomo katika riwaya hii ni tamaa iliyooneshwa kupitia Salihi na Majivuno, Unafiki na woga wa wananchi wa kusadikika, utengano na kukosekana kwa umoja. 

Migogoro. Hali ya kutoelewa au kuridhishwa na jambo fulani na kupelekea kutoelewana kwa makundi au pande mbili za watu. Katika riwaya hii kuna migogoro ya kijamii, kisiasa na kiuchumi. 

Migogoro ya kijamii. Mfano wa migogoro ya kijamii ni mgogoro wa Sapa na Salihi uliotokea baada ya Sapa kuomba upofu kutokana na tama ya Salihi kutamani vitu vya Sapa, Mwandishi anasema “kwa sababu hii tuliafikiana kushirikiana kila kitu atakachoomba tukaandikiana hati mbele ya Kadhi. Palepale mwenzangu aliinua mikono yake juu akaomba upofu” uk.30 

Mgogoro nafsia: ni hali ya mtu kuhofia jambo fulani na kupelekea mtu huyo kuwa namsongo wa mawazo, Mwandishi amemtumia waziri Majivuno aliyekuwa na hofu ya kupoteza madaraka na kukomeshwa kwa ukandamizaji endapo wananchi wataelewa sheria mbalimbali za kusadikika waliokuwa wakielimishwa na Karama. Hatimaye aliamua kumshitaki katika baraza msanii anasema “Upelelezi huo ulidhihirisha bila ya shaka yoyote kuwa mshitkiwa akiwafunza watu sio kuomba msamaha na huruma katika baraza tu lakini hata kuzibatilisha hukumu za baraza la kusadikika kwa njia zote hii inaonesha kuwa mgogoro mkubwa utakuwako kati ya sheria za nchi na watu wake” uk 2. 

Migogoro ya Kiuchumi. Mgogoro wa walionacho/matajiri ambao ndio waliopewa haki na upendeleo na Maskini walionyimwa haki hata mbele ya sheria na mahakaka.Katika nchi ya kusadikika watu hawa hawakuweza kabisa kushirikiana.Mwandishi anasema “Aghalabu Mashitaka mengi yalikubaliwa bila ya swali wala kiapo kama mashitaka yaliletwa mbele ya baraza na wafalme, watoto wao, matajiri au watu wengine maarufu nguvu ya desturi hii ilifanywa maradufu. Hapana shaka salama ya watu wadogo ilikuwa kidogo sana katika nchi ya kusadikika” uk. 7. 

Migogoro wa Kisiasa. Huu ni mgogoro unaowahusisha wanaharakati wazalendo walioongozwa na karama dhibi ya serikali na viongozi wan chi ya kusadikika. Wanaharakati hao walihitaji mabadiliko na walichoshwa na uonevu wa viongozi wao, mgogoro huu ndio uliopelekea wananchi kuishia kifungoni pindi walipojitolea kudai mabadiliko. 

Ujumbe. Uongozi mbaya unachangia kwa kiasi kikubwa kukwamisha maendeleo ya wananchi. Kuwepo kwa hali ya uzalendo katika nchi ni chachu ya maendeleo na mafanikio katika jamii. Suala la uelimishaji (elimu) ni muhimu katika utambuzi wa wananchi katika shughuli mbalimbali za kijamii.Tamaa na viongozi kujali maslahi kunapelekea hali duni ya wananchi walio wengi. Viongozi wanapaswa kuthamini haki za wananchi wanaowatumikia. 

Msimamo wa Mwandishi. Msimamo wa mwandishi katika riwaya hii ni wa kimapinduzi kwani anaonesha jinsi jamii ilivyopaswa kujituma tena kwa ujasiri, kupigania haki na mabadiliko ya wananchi wote. 

Mtazamo wa Mwandishi. Mtazamo wa mwandishi wa riwaya hii ni wa Kiyakinifu kwani kwa kiasi kikubwa umeakisi mambo ambayo yanaweza kufuatwa katika kufanikisha maendeleo ya jamiii yeyote kama vile mgongano wa mawazo uzalendo na ujasiri, uelewa na mambo mengine. Aidha yapo baadhi ya maeneo yanagusia mtazamo wa kidhanifu kama vile kusadiki kila kinachosemwa na watawala. 

Falsafa ya mwandishi. Falsafa ya mwandishi ni ya wema hushinda ubaya, amedhihirisha hili kupitia mhusika Karama aliyechorwa kama mtu mwema dhidi ya Majivuno aliyechorwa kama mtu mbaya. Kwa taswira hii Karama amewakilisha wema wote katika jamii ya wasadikika na Majivuno anawakilisha wabaya wote katika jamii hiyohiyo

Comments

Popular posts from this blog

KISWAHILI FORM 1: FASIHI SIMULIZI

KISWAHILI Form 1 Topic 4 FASIHI SIMULIZI Fasihi simulizi ni moja kati ya tanzu za fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo. Katika mada hii utajifunza na kisha utaweza kubainisha tanzu na vipera vya fasihi simulizi pamoja na ufafanuzi wake. Na pia utaweza kutofautisha kati ya kipera na kipera au kati ya utanzu na utanzu. Ubainishaji wa Tanzu za Fasihi Simulizi Tanzu za Fasihi Simulizi Bainisha tanzu za fasihi simulizi Fasihi Simulizi ni kazi ya fasihi inayohifadhiwa na kurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mdomo kama vile; hadithi, ngoma na vitendawili. Tanzu za Fasihi Simulizi ni pamoja na hizi zifuatazo: Masimulizi/hadithi Semi Ushairi Mazungumzo Maigizo Ngomezi Ufafanuzi wa Vipera vya Tanzu za Fasihi Simulizi Vipera vya Hadithi Fafanua vipera vya hadithi SIMULIZI/ HADITHI Masimulizi ni fasihi yenye kusimulia habari fulan...

NOTES ZA USHAIRI

USHAIRI     NI    NINI ? Shaaban Robert katika uandishi wa ushairi ameandika Tenzi na mashairi ya kimapokeo. Tenzi : Ni aina ya mashairi ya kimapokeo wenye sifa zifuatazo: Kimaudhui ; Ni utungo wenye maudhui yanayosimulia kwa urefu tukio fulani maalum. Waweza kuwa wasifu wa mtu au jambo la kihistoria. Mfano; S. Robert ameandika utenzi wa vita vya Uhuru, ameeleza kuhusu historia. Pia katika Mapenzi Bora, ameeleza kuhusu sifa za mapenzi bora. Utenzi ni utungo wa pili kati tungo za ushairi zenye beti nyingi. Utungo wa kwanza unaoongoza kuwa na beti nyingi kuliko zote katika ushairi ni Tendi. Lakini hapa tutaangazia tenzi zaidi. Utenzi hauna mizani nyingi aghalabu mizani nane, hauna mshororo bali una nusu mshororo/kipande mstari. Vilevile katika utenzi kipande mstari hakigawiki. Pia katika kipande mshororo kuna vipande vinne kwa kila ubeti. Mistari mitatu ya kwanza huwa na vina vyenye urari na kipande mstari cha mwisho/cha nne huwa...

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...