Skip to main content

SHAIRI: IWE CHUNGU IWE TAMU

Kwetu ulimi maneno,mengine ni ya ziada,
Siye twatoa misemo,na nyimbo kwenye ibada,
Ladha kwetu siyo somo,ladha kwetu siyo shida,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.


Vya maana twaviona,twanusa na kusikia,
Hizo suti za kushona,na vingi vya kuvutia,
Tulivitamani sana,tumeshindwa kufikia,
Iwe chungu iwe tamu, cha msingi ni kushiba.

Iwe biringanya mbichi,ama pilipili manga,
Karoti ama kabichi,ama dagaa mchanga,
Sie milo haichoshi,tunatamani kusonga,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.

Sie hatuna ratiba,tupatacho tunakula,
Tunachopenda kushiba,hatuchagui vyakula,
Bila soda tunashiba,tunakula kisha sala,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.

Kwetu hatuna jokofu,hatuchachishi viporo,
'Tabaki na yako hofu,utumbo hauna kasoro,
Kunenepa hatuhofu,leo twala kesho doro,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.

Si kwamba hatutamani,tamaa twaweka ndani,
Twapiga kazi jamani,siku tuwe na vyetu ndani,
Maisha hatulingani,tajiri na masikini,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.

Shughuli na matukio,twajua chungu na tamu,
Jaani ndo kimbilio,kama vile si timamu,
Njaa huleta kilio,hatujui neno hamu,
Iwe chungu iwe tamu,cha msingi ni kushiba.

Comments

Popular posts from this blog

MBINU ZA KUFUNDISHIA

Mbinu za kufundishia , ni miongozo mbalimbali atumiayo mwalimu wakati wa kufundisha somo aliloliandaa kwa wanafunzi wake. Walimu wanapaswa kuamua kwa kuchagua kwa makini njia na mbinu bora za kufundishia ili wanafunzi wake waweze kujifunza kwa ufanisi. Ziko njia nyingi za kutengeneza mazingira ya mtoto aweze kujifunza na pia ziko mbinu nyingi za kufundishia. Pamoja na wingi huo tunaweza kuzigawa katika makundi makuu mawili kadri ya jinsi zinavyowashirikisha watoto katika tendo la kujifunza, ambazo tunaweza kuziita shirikishi na zisizo shirikishi . Zifuatazo ni baadhi ya mbinu shirikishi na zisizo shirikishi za kufundishia pamoja na faida na hasara zake:- Njia ya majadiliano , njia hii imekuwa ikitumika katika ufundishaji kwa muda mrefu. Katika kujadiliana mwanafunzi mmoja mmoja hupata nafasi ya mawazo aliyonayo kuhusu suala linalojadiliwa na yeye pia huweza kupata mawazo yaw engine. Katika majadiliano mwanafunzi hupata ujuzi mpya nje na ule aliokuwa nao kabla hajashiriki kat...

NOTES ZA USHAIRI

USHAIRI     NI    NINI ? Shaaban Robert katika uandishi wa ushairi ameandika Tenzi na mashairi ya kimapokeo. Tenzi : Ni aina ya mashairi ya kimapokeo wenye sifa zifuatazo: Kimaudhui ; Ni utungo wenye maudhui yanayosimulia kwa urefu tukio fulani maalum. Waweza kuwa wasifu wa mtu au jambo la kihistoria. Mfano; S. Robert ameandika utenzi wa vita vya Uhuru, ameeleza kuhusu historia. Pia katika Mapenzi Bora, ameeleza kuhusu sifa za mapenzi bora. Utenzi ni utungo wa pili kati tungo za ushairi zenye beti nyingi. Utungo wa kwanza unaoongoza kuwa na beti nyingi kuliko zote katika ushairi ni Tendi. Lakini hapa tutaangazia tenzi zaidi. Utenzi hauna mizani nyingi aghalabu mizani nane, hauna mshororo bali una nusu mshororo/kipande mstari. Vilevile katika utenzi kipande mstari hakigawiki. Pia katika kipande mshororo kuna vipande vinne kwa kila ubeti. Mistari mitatu ya kwanza huwa na vina vyenye urari na kipande mstari cha mwisho/cha nne huwa...

DHANA YA MATUMIZI YA LUGHA, REJESTA, UTATA

Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Katika mada hii utajifunza mambo ya msingi ya kuzingatia unapotumia lugha. Utaelewa dhana mbalimbali zinazohusishwa na matumizi ya lugha kama vile rejesta, misimu, utatata katika lugha, lugha ya mazungumzo na lugha ya maandishi. Matumizi ya lugha ni namna ambavyo wazungumzaji wa lugha hutumia lugha kwa kuzingatia mila, desturi na kaida mbalimbali za jamii inayohusika. Dhima ya matumizi ya lugha Dhima kuu ya lugha ni kupashana habari, ujuzi na maarifa mbalimbali. Vilevile lugha husaidia kujenga uhusiano mwema baina ya watu. Uhusiano huo unaweza kuwa wa kijamii, kielimu, kibiashara, kihuduma, kisiasa, kiuchumi n.k. Kwa hiyo, kujua jinsi ya kuitumia lugha kama inavyotakiwa, kunasaidia kufikisha vizuri ujumbe unaotakiwa bila kuupotosha. Vilevile kunasaidia kuepuka migongano, hasa ya kijamii kwa kuwa utakuwa umetumia lugha kwa mujibu wa mi...